Kwa mujibu wa Shirika la Habari la Kimataifa la Ahlul-Bayt (as) -ABNA-, Kamati ya habari ya timu ya mazungumzo ya "Minab 168" imechapisha taarifa ya makubaliano muhimu yaliyofikiwa katika duru ya kwanza ya mazungumzo yaliyofanyika Bürgenstock nchini Uswisi.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo, shinikizo kutoka kwa timu ya mazungumzo ya Iran lilisaidia kudumisha usitishaji wa mapigano nchini Lebanon, huku kukikubaliwa kuundwa kwa utaratibu wa ufuatiliaji uitwao Kitengo cha Usimamizi wa Migogoro (Conflict Management Unit) ambao utahusisha ushiriki wa Iran katika masuala ya usalama wa Lebanon.
Aidha, pande hizo zimekubaliana kuanzisha njia maalumu ya mawasiliano ya dharura kuhusu usimamizi wa Mlango wa Hormuz ili kuhakikisha njia hiyo muhimu ya bahari inaendelea kufunguliwa hatua kwa hatua, jambo ambalo taarifa hiyo inalieleza kuwa linathibitisha nafasi ya Iran katika usimamizi wa eneo hilo.
Taarifa hiyo pia imeeleza kuwa timu za pamoja zitakazoshughulikia masuala ya mpango wa nyuklia, vikwazo na ufuatiliaji zitaanza kazi baada ya kutekelezwa kwa masharti ya kusitisha mapigano katika maeneo yote ya mapambano, hususan Lebanon, pamoja na kuanza kuondolewa kwa mzingiro wa baharini, kuachiliwa kwa mali za Iran zilizokuwa zimegandishwa na kuanza kutekelezwa kwa uamuzi wa kuondoa vikwazo dhidi ya sekta ya mafuta na petrokemikali.
Vilevile, Iran na Qatar zilisaini hati ya makubaliano kuhusu utekelezaji wa mpango wa kuachiliwa kwa mali za Iran zilizokuwa zimezuiliwa nje ya nchi.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo, Ofisi ya Udhibiti wa Mali za Kigeni (OFAC) ya Wizara ya Hazina ya Marekani pia ilitoa nyaraka zinazoruhusu kusitishwa kwa vikwazo dhidi ya sekta ya mafuta, petrokemikali na bidhaa zake kwa muda wa siku 60, hatua inayoruhusu Iran kuuza mafuta yake kupitia njia rasmi na kupokea mapato kupitia Benki Kuu ya Iran.
Your Comment